Uongozi wa Simba SC umefichua Siri ya Mafanikio katika Michuano ya Kimataifa, baada ya kufanikiwa kurejea Hatua ya Makundi Ligi ya Mabingwa Barani Afrika msimu huu 2022/23.

Simba SC ilitinga hatua hiyo Jumapili (Oktoba 16) kwa ushindi wa 1-0, ambao unaifanya klabu hiyo kupata ushindi wa jumla wa mabao 4-1, baada ya kushinda ugenini Luanda-Angola 1-3, Oktoba 09.

Mjumbe wa Bodi ya Wakurugenzi ya Klabu hiyo Mulamu Ng’ambi amesema kuweka malengo na kuyafanyia kazi kwa vitendo, imekua sehemu kubwa ya kufanikiwa katika mpango huo.

Mulamu amesema kwa miaka mitano mfululizo Simba SC imefika katika hatua hiyo mara tatu upande wa Ligi ya Mabingwa Barani Afrika na mara moja Kombe la Shirikisho, kutokana na kutambua nini kinachohitajika kwenye Michuano hiyo inayoratibiwa na Shirikisho la Soka Barani Afrika ‘CAF’.

Amesema kuwa na kikosi bora na imara imeifanya Simba SC kuwa kwenye mazingira mazuri ya kucheza soka la ushindani na sasa imekua na kikosi ambacho kina uwezo wa kushinda popote Barani Afrika, tofauti na ilivyokua misimu iliyopita.

“Kuna maendeleo makubwa sana kwenye kikosi chetu ukiangalia misimu iliyopita hadi hapa tulipofikia, kuna mengi yamefanyika kataka usajili wa wachezaji ambao wana uwezo wa kucheza Michuano hii ya Afrika”

“Tumekua makini sana katika usajili wa hawa wachezaji, tumekua tukiangalia wapi tunapokosea na kujirekebisha kwa haraka, hii ndio siri kubwa ya kupata mafanikio haya katika miaka hii mitano, tangu tulipoingia kwenye mfumo wa mabadiliko ya kiutendaji chini Mwekezaji Mohamed Dewji ‘Mo’, 

“Leo hii Simba SC kwenda kupata ushindi ugenini katika michezo miwili mfululizo limedhihirisha ukomavu wa kikosi chetu na aina ya wachezaji tuliowasajili ni vipi wapo tayari kupambana, kwa hiyo tumepiga hatua kubwa sana.” amesema Mulamu Ng’ambi

Katika mchezo wa Mzunguuko wa Kwanza Ligi ya Mabingwa Barani Afrika msimu huu Simba SC ilishinda mjini Lilongwe-Malawi 0-2 dhidi ya Nyassa Big Bullet, huku ikifanya hivyo tena Luanda-Angola kwa kuichapa CD Primeiro de Agosto mabao 1-3 kwenye mchezo wa Mzunguuko wa Pili.