Header Ads

Header ADS

Kijiji cha Usetule na Mahongole katika Halmashauri ya Makambako Mkoani Njombe vya pata maji ya Bomba

  Zaidi  ya wakazi 5,463 wa vijiji vya Usetule na Mahongole Halmashauri ya Mji Makambako mkoani Njombe,wameondokana na kero ya huduma ya maji safi na salama kufuatia wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini(Ruwasa)wilaya ya Njombe kukamilisha  ujenzi wa mradi wa maji Mahongole.

Akizungumza na Waandishi wa Habari waliotembelea mradi huo,mwenyekiti wa chombo cha watoa huduma ya maji ngazi ya jamii(CBWSO)Boniface Gadau alisema,chanzo kikuu cha maji  kipo kijiji cha Kichiwa na huduma ya maji inatolewa kwa masaa 24.

Alisema,chombo kinasimamia vituo 28 vya kuchotea maji pamoja na wateja waliounganishiwa huduma hiyo majumbani na taasisi za umma ambavyo vyote vimefungiwa dira/mita.

Alieleza kuwa,chombo kina matenki mawili yenye uwezo wa kuhifadhi lita 150,000 za maji  na wasimamizi wote wa chombo na mradi huo wamepata mafunzo ya usimamizi wa mradi,kama sehemu ya kuwajengea uwezo kutoka kwa wataalam wa Ruwasa wilaya ya Njombe.

Gadau alitaja vyanzo vikuu vya mapato vya CBWSO ni tozo za maji zinazoptikana kutoka kwenye vituo vya kuchotea maji,tozo kutoka kwenye taasisi ambapo fedha  zinazopatikana zinasaidia kumudu gharama za uendeshaji wa mradi huo.

Kwa upande wake katibu wa CBWSO hiyo Philimon Nganilevando alisema,bei ya maji zinazotumika ni zile zilizoidhinishwa na wizara ya maji kulingana na teknolojia ya mserereko inayotumika kwenye vijiji husika ambayo ni Sh,1,000 kwa unit 1.

Alisema,kwa mara ya kwanza chombo kimeanza kukusanya tozo za maji mwezi Novemba 2022 ambapo mapato yalikuwa Sh.361,500  na kinadai Sh.90,000 kati ya hizo Sh.40,000 ni deni la taasisi za serikali.

Alisema,tangu chombo kilipoanzishwa wamepata mafanikio mengi ikiwamo kutoa elimu kwa jamii juu ya umuhimu wa kulipia huduma ya maji,matumizi bora ya maji,utunzaji wa miundombinu,mazingira na namna ya kukusanya fedha kwa wateja wake.

Nganilevando,ameishukuru serikali kupitia wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini(Ruwasa), kujenga mradi huo kwani umesaidia kumaliza kabisa changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji  kwa wananchi wa vijiji hivyo iliyokuwepo kwa muda mrefu.

Kaimu meneja wa Ruwasa wilaya ya Njombe Bakari Kitogota alisema,baada ya kukamilika kwa mradi huo sasa wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama  karibu na  makazi yao na kuwawezesha kushiriki kazi zote za maendeleo na ujenzi wa Taifa.
Baadhi ya viongozi wa serikali ya kijiji cha Mahongole na Usetule wilayani Njombe wakiangalia sehemu ya miundombinu ya maji iliyojengwa kwa ajili ua kuhudumia wakazi wa vijiji hivyo na wakala wa maji na usafi wa nmazingira vijijini(Ruwasa) wilaya ya Njombe.
Tenki la kuhifadhi maji linalohudumia wakazi wa kijiji cha Mahongole na Usetule Halmashauri ya mji Makambako wilayani Njombe.

 

No comments

Powered by Blogger.