Header Ads

Header ADS

Serikali kuingiza Umeme Vijiji 74 Singida

               Vijiji 74 wilayani Ikungi mkoani Singida vinatarajia kupata umeme wa Wakala wa Umeme vijijini (REA) ifikapo mwaka 2020.Hayo yamesemwa na Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Edward Mpogolo wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Irisya katika mkutano wa hadhara alipofanya ziara ya kukagua miradi na kujitambulisha baada ya kuteuliwa na Rais Dkt. Johh Magufuli kuwa DC wa wilaya hiyo.

Vijiji 74 katika wilaya yetu vitapata umeme wa REA awamu ya tatu hivyo jiandaeni kuanzisha viwanda vidogo vidogo kwani hiyo ni fursa kwenu” alisema Mpogolo.

Mpogolo alisema katika wilaya hiyo kuna vijiji 101 na kata 28 na  makao makuu zilipo kata hizo karibu zote tayari zimepata umeme kasoro chache na dhamira ya Rais  Dkt. John Magufuli nikuona ifikapo mwaka 2020 vijiji vyote na vitongoji vinakuwa na umeme.

Wakizungumza katika mkutano huo wananchi hao walieleza changamoto mbalimbali kubwa ikiwa ni kuwa na daktari mmoja katika Kituo cha afya katika kata hiyo hali inayoleta usumbufu pale anapopata dharura.

” Tunakuomba DC wetu utusaidie tupate daktari na muuguzi katika zahanati yetu ambayo inauhaba wa watumishi baada ya waliokuwepo kuhamishwa na kubaki mmoja” alisema Jumanne Mohammed.

Samuel Mathayo alisema kutokana na zahanati hiyo kutoa huduma kwa vitongoji vingine vilivyo jirani na Irisya aliomba ipandishwe hadhi  na kuwa kituo cha afya ili kukabiliana na wingi wa wagonjwa.

Kwa upande wake Simoni Muna aliomba ujenzi wa madarasa ya Shule ya Msingi Munyu ukamilike haraka ili kuwapunguzia adha ya kutembea zaidi ya kilometa tatu watoto wanao ishi katika eneo hilo kwenda kusoma Shule ya Msingi ya Irisya.

Mkazi mwingine wa kata hiyo Iddi Ikuja aliiomba serikali kusaidia kutatua migogoro ya ardhi ambayo ni mingi inayosababishwa na watu kuvamia mashamba ya wenzao wakidai ni yao.

Juma Mbihaji alitaka kujua  serikali inampango gani wa kutoa ajira kwa watoto wao ambao wamemaliza masomo  lakini wapo kijijini hapo mwa muda mrefu bila ya kuwa na kazi.

Diwani wa kata hiyo Ally Mwanga aliomba mradi wa maji uliopo katika kata hiyo uharakishwe ili uanze kufanya kazi kwa kununua mabomba na vifaa vya usambazaji.

“Tayari serikali ilikuja kupima maji na kufanya majaribio ambapo maji yalitoka kwa wingi na kuleta furaha kwa wananchi kwani tangu kata hii ianzishwe hatujawahi kuwa na bomba la maji zaidi ya kutumia ya visimani” alisema Mwanga.

Alisema maji yaliyopatikana yanauwezo wa kutoa lita 18,000 kwa saa ambapo ni sawa na pipa 740 na kuwa kata hiyo itajitosheleza na ziada itakwenda katika vitongoji vingine vya jirani vya Munyu na Masutianga.

No comments

Powered by Blogger.