Header Ads

Header ADS

RC Shigella azindua Rasmi Kampeni ya kujiunga na Bima ya Afya

    MKUU wa Mkoa wa Tanga Martin Shigella amezindua rasmi kampeni ya uhamasishaji wananchi kujiunga na vifurushi vya Bima ya Afya kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga huku akitoa maelekezo kwa Wakuu wa wilaya za mkoa huo na Meneja wa NHIF Mkoa huo Ally Mwakababu kuhakikisha wanafanya uzinduzi kwenye ngazi ya wilaya.

   Shigella aliyasema hayo kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga wakati wa uzinduzi huo ambapo aliipongeza NHIF kwa uamuzi wa kuja na vifurushi ikiwemo kufanya uzinduzi kwa kila mkoa ambao ni ubunifu mkubwa sana wanaoufanya na utawasaidia watanzania wengi kujiunga na mfuko huo.
  Aidha ,Mkuu huyo wa mkoa aliipongeza pia bodi ya NHIF kwa kuwa na ushirikiana mkubwa wa kufanya shughuli zao kwa ufanisi mkubwa unaowezesha mfuko huo kupiga hatua kubwa za kimaendeleo ikiwemo kutoa huduma nzuri kwa watanzania.
  “Mimi nakufahamu vizuri sana Mwenyekiti wa Bodi kwa kazi nzuri ambazo unafanya kila mahala unapokabidhiwa hakujawahi kulegalega wala kurudi nyuma kunasonga mbele tena kwa kasi kubwa na mafanio hongera mama kwa kazi nzuri lakini pia niipongeze bodi ya NHIF”Alisema
  Hata hivyo Mkuu  wa mkoa huyo aliipongeza bodi ya mfuko huo kwa kazi nzuri ambao wamekuwa wakiifanya hata wanapokwenda mikoani kufuatilia maendeleo ya mfuko huo wamekuwa na ushirikiano mkubwa ambao umekuwa na tija kubwa kwa maendeleo.
  “Lakini nipongeza Menejimenti chini ya Mkurugenzi wao Benard Konga wamekuwa wakifanya kazi kubwa katika kutimiza majukumu yao kwa kujituma ndio maana taarifa niliyoipata ni kwamba katika mifuko inayoenda vizuri na wanachama wanapata huduma kwa wakati na gharama zinazotokana na wanachjama kupata huduma za afya zinalipwa kwa wakati ni pamoja na NHIF”Alisema
  Hata hivyo aliwaagiza wamiliki wa viwanda kuhakikisha wanawaingiza kwenye mpango wa huduma ya bima za afya vibarua wanaofanya shughuli za uzalishaji katika viwanda ili waweze kuwa na uhakika wa matibabu yao na familia zao.
  Alisema kwamba mojawapo ya kundi lililo sahaulika ni vibarua toka viwandani ambao kwa sasa wanafikiria waingizwe kwenye mpango huo ili wakati wanapougua waweze kuwa na uhakika wa matibabu
  Mkuu huyo wa mkoa alisema kundi hilo linafanyakazi kubwa ya uzalishaji lakini lipo kwenye mazingira magumu ya kazi zao huku hawajui hatma ya afya zao pamoja na familia zinazowategemea kutokana na kutokuwepo kwenye mfumo huo ambao unawawezesha kupata matibabu kwa njia ya Bima ya Afya.
  “Jambo lililoanzishwa na NHIF la vifurushi vya bima ya afya ni jema sasa …nawaagiza MaDC na wamiliki wa viwanda wekeni utaratibu mzuri kwa vibarua wote wanapatiwa huduma hii ili kuwanusuru na afya zao” Shigella alisema.
  Mwanzo akizungumza katika uzinduzi huo Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa NHIF Anna Makinda alisema ni mfumo bora ulioanzishwa na mfuko huo ambao unaweza kuyasaidia makundi mengi ambayo yalikosa fursa ya kupata huduma hiyo ya afya.
   Makinda alisema awali mfuko huo uliwajali watumishi wa umma pekee huku asilimia kubwa ya watanzania ambao si watumishi hawakuwa na nafasi ya kujiunga na mfuko huo jambo ambalo ni hatari kwa ustawi wa afya walizo nazo.
  “Yapo makundi kama bodaboda,machinga,na sacos mbalimbali ambazo hazikunufaika na huduma hii lakini kupitia mfumo huu wa vifurushi naamini kila mmoja anaweza kujiunga na kunufaika ili kwajengea uhakika wa matibabu yao”Alieleza.
  Sanjari na hayo pia alisema tayari walishakubaliana na benki ya NMB ili kutoa mwanya kwa wananchi walio na kipato cha chini waweze kulipa kidogokidogo ili waweze kujiunga na huduma hiyo.
  Naye kwa upande wake Mkurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Benard Konga alisema kwamba watanzania asilimia 34 ndio wapo kwenye mfumo wa bima ya afya bado safari ni ndefu kuhakikisha kila mtanzania anaingia kwenye bima ya Afya.
  Alisema pia mfuko mwaka hadi mwaka mapato yamezidi kuongezeka na kuanzia mwaka 2014/2015 hadi kufikia sasa yameongezeka asilimia 33 hivi sasa wanakusanya Bilioni 502 kutoka kwa wanachama wao.
 Alisema mchango wao kwenye sekta ya afya umeongezeka ambapo kwa mwaka wanalipa mpaka bilioni 441 ambazo wanatuma kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.


No comments

Powered by Blogger.