Header Ads

Header ADS

GLISTEN YAPONGEZWA KWA KUSHIKA NAFASI YA KWANZA MANYARA

Shule ya Awali na Msingi Glisten International ya Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara imezidi kufagiliwa kwa kuongoza kwa ufaulu wa matokeo ya darasa la nne kwa mkoa huo. 
 Shule ya Glisten kwa mujibu wa matokeo ya darasa la nne ya mwaka 2019 imeshika nafasi ya kwanza kwa Wilaya ya Simanjiro, ya kwanza pia kwa mkoa wa Manyara na ya 39 kitaifa kwa shule zote za msingi 3,244 za Tanzania. 
    Mkurugenzi wa shule ya Glisten, Justin Mirisho Nyari alisema anawazawadia walimu wanne waliowafundisha wanafunzi wa darasa la nne wa mwaka jana shilingi laki moja kila mmoja kama zawadi ya matokeo hayo. 
Pia Mh Nyari  Mwenyekiti wa chama cha wachimbaji madini Mkoa wa Manyara (Marema) na mheshimiwa diwani mstaafu wa Kata ya Mirerani aliwaahidi wanafunzi 30 wa taaluma ya michezo kuwanunulia sare za michezo kutokana na vipaji walivyonavyo. 
Alieleza kuwa lengo la kuanzisha na kuwekeza kwenye shule hiyo iliyopatiwa usajili mwaka 2017 ni kuhakikisha watoto wa eneo hilo wanapata elimu bora. 
"Tunamuunga mkono Rais John Magufuli kwa kuwekeza kwenye sekta ya elimu kwani tumeona juhudi zake za kusimamia maendeleo ikiwemo kujenga ukuta unaozunguka migodi ya madini ya Tanzanite ili kulinda rasilimali hiyo muhimu," alisema. 
Hata hivyo, Ofisa elimu ya watu wazima wa halmashauri ya wilaya ya Simanjiro, Lazaro Tibaigana aliwataka walimu na wanafunzi wa shule hiyo kutobweteka na ushindi huo kwani shule nyingine nazo zinalengo la kushika nafasi ya kwanza kimkoa. 
"Mmetupa heshima kubwa wilaya ya Simanjiro kwa kuongoza kwenye mkoa wa Manyara hivyo kazeni buti zaidi ili muongoze tena," alisema. 
Miongoni mwa wanafunzi wa shule hiyo Magreth Leons Kimario alisema wanamuombea Mkurugenzi wa shule hiyo Justin Nyari kwa Mungu ili aweze kuendeleza shule yao. 
"Pia tunawaombea walimu na wazazi wetu waweze kutimiza majukumu yao ipasavyo na kusababisha sisi tofauti mitihani yetu kupitia masomo tunayofundishwa," alisema. 
Kwa mujibu waMwalimu mkuu wa shule hiyo Sabato Joshua alisema katika tafrija hiyo wanafunzi wa darasa la nne wa mwaka jana walipatiwa zawadi ya vyeti na vitabu kwa kila somo walilochagua. 
Aidha, ili kuonyesha umoja na upendo, baadhi ya walimu wa shule ya awali na msingi New Vision ya mji mdogo wa Mirerani, walishiriki pamoja kwenye tafrija hiyo. 


No comments

Powered by Blogger.