Header Ads

Header ADS

Waziri wa Israel akabiliwa na tuhuma za ufisadi.

  Kesi inayomkabili Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ambayo ilikuwa inasubiriwa kwa muda mrfeu, inatarajiwa kusikilizwa Machi 17, kwa mujibu wa vyanzo rasmi kutoka nchini humo.
  

  Waziri Mkuu wa Israel anakabiliwa na mashitaka ya ufisadi, ulaghai na uvunjaji wa imani katika kesi tatu tofauti. Tarehe hiyo imetangazwa Jumanne wiki hii na Wizara ya Sheria.
 Jumanne ya wiki hii Benyamin Netanyahu alipokea mwaliko binafsi kutoka mahakama ya Jerusalem. Waziri Mkuu wa Israel anatakiwa afike mahakamani Machi 17, wakati wa ufunguzi wa kesi yake kwa kusomewa mashtaka yanayomkabili.
  Mwezi Novemba, Waziri Mkuu alishitakiwa na mwanasheria mkuu kwa kutoa hongo, kufanya udanganyifu na kuwavunja imani raia waliomchagua kuhusiana na kesi tatu tofauti.
  Netanyahu ambaye ni kiongozi wa muda mrefu wa nchi hiyo alidaiwa kukubali kuchukua zawadi kutoka kwa wafanyabiashara matajiri na kutoa hongo ili kuweza kuwa katika vyombo vya habari mara dufu.
  Aidha Bw. Netanyahu atakuwa Waziri Mkuu wa kwanza katika historia ya Israeli kufikishwa mbele ya mahakama nchini humo.
  Kesi hii itaanza wakati mazungumzo ya kisiasa yatakuwa yanaendelea kwa lengo la kuunda serikali mpya. Benyamin Netanyahu amepata ahadi mpya kutoka kwa washirika wake wa mrengo wa kulia wa kumuunga mkono katika hatua hii. Lakini mkataba huu utadumu hadi lini?Kuna hatari kuwa picha za yeye kuwa mahakamani zitamdhofisha kisiasa.
  Hata hivyo, Siku ya Jumanne, mpinzani wake mkuu Benny Gantz alisema katika mkutano wa kampeni yake kwamba kuanzia Machi 17, "Netanyahu atajihusisha tu na kesi yake. Hataweza kusimamia masilahi ya raia wa Israeli, "alisema.
 Naibu Waziri wa Ulinzi, mwanachama wa Likud, chama cha Benyamin Netanyahu, anaamini, kwa upande wake, kwamba Benyamin Netanyahu anaweza kusimamia kesi yake na kutekeleza jukumu lake kama Waziri Mkuu.
  Chaguzi zilizopita zilizofanywa mwezi Aprili na Septemba mwa 2019 zilikifanya chama cha Bw. Netanyahu cha mrengo wa kulia cha Likud kujikuta kwenye njia panda dhidi ya chama Blue na White hali iliyokifanya kushindwa kuunda serikali.
  Changamoto za kisheria zinazomkabili Bw. Netanyahu zimekuwa kikwazo katika majadiliano. Amekuwa akisisitiza kuwa mashtaka hayo ni jaribio la mapinduzi dhidi yake.

No comments

Powered by Blogger.