Header Ads

Header ADS

Tundulissu ataka mchakato wa Katiba Mpya uanzie pale ulipoishia mchakato wa tume ya Jaji Warioba

 Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Bara), Tundu Lisu amependekeza mchakato wa Katiba mpya uanzie pale ulipoishia kama ulivyoanzishwa na Tume ya Jaji Warioba.
Alisema kisheria Katiba iliyopendekezwa na iliyokuwa Tume ya Warioba muda wake uliisha na kuna vipengele ambavyo vinahitaji kurekebishwa, ili viweze kuendana na matakwa ya Watanzania kulingana na karne iliyopo.
Akihutubia wanachama wa kanda ya Kaskazini kupitia mtandao wa zoom katika ukumbi wa Shaaban Robert jijini Tanga, Lissu, anayeishi nchini Ubelgiji alisema ni vyema harakati za kudai Katiba zikaanzia pale ulipoishia mchakato wa Katiba ya tume ya Warioba.

Alisema licha ya kuwa Katiba iliyopendekezwa na Warioba ni nzuri, lakini ina vipengele ambavyo havina tofauti na iliyopo hivi sasa ambayo inawapa nguvu watawala.
Aliwaomba Watanzania kuungana mijini na vijijini kuwa sauti moja itakayowezesha mchakato wa Katiba mpya kufikiwa.
“Mchakato huu si wa viongozi wa Chadema au CCM pekee, bali unahitaji kuwa na nguvu ya umma ya pamoja,” alisema Lissu.
Kuhusu yeye kurejea Tanzania, alisema kwa kuwa kilichomkimbiza nchini Tanzania na kwenda Ubelgiji ni suala la usalama wake, ikiwamo kupigwa risasi na kunusurika kukamatwa mara baada ya uchaguzi wa mwaka 2022, anasubiri mazingira ya usalama wake yawekwe wazi.
“Nina imani kwamba mazingira ya mimi kurejea Tanzania yatakuwa mazuri, kwa sababu hata mazungumzo yanayoendelea baina yetu na Serikali sehemu nyingine yanahusiana na uwekaji wa mazingira ya mimi kurejea nchini kwangu....yakiwa mazuri nitarejea haraka kwa sababu kutoka huku na Tanzania ni saa chache,” alisema Lisu.
Lema ataja kilichomkimbiza
Naye Mwenyekiti wa Chadema kanda ya Kaskazini, Godbless Lema alieleza madhila yaliyosabisha aende Canada kuwa aliona ni vyema kuokoa maisha yake kuliko kuendelea kuishi Tanzania.
“Ninaposikia wakimbizi nafika mbali sana kwa sababu mimi ni miongoni mwa walioonja machungu ya ukimbizi; hakuna kitu kizuri kama kuishi nchini kwako ukiwa na ndugu zako,” alisema Lema.
Hata hivyo, Lema alisema yupo katika mchakato wa kurejea Tanzania baada ya kuridhishwa na mazingira ya usalama yaliyowekwa.
“Nimeshazigawa hata nguo zangu za baridi ya huku nje, narejea Tanzania na sitarejea kinyonge; nakuja na nguvu mpya ya kupambana,” alisema Lema.
Aidha, aliwaomba Watanzania kuungana kupigania njia sahihi ya utawala bora kwa kupata katiba itakayomwajibisha yeyote atakayefanya makosa.
Kongamano hilo lilihudhuriwa na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Benson Kigaila na aliyekuwa diwani wa kata ya Mwanzange kupitia CUF na baadaye kuhamia ACT Wazalendo, Rashid Jumbe.
Jumbe amejiunga na Chadema akisema sababu iliyomvuta ni harakati za kweli za kudai Katiba mpya.
“Nimekuja Chadema na kundi kubwa la waliokuwa wanachama wa ACT Wazalendo, hatukuja kutaka uongozi, bali kuimarisha mapambano ya Katiba mpya,” alisema Jumbe, ambaye ni miongoni mwa mwanasiasa wenye umaarufu jijini Tanga.


No comments

Powered by Blogger.