Header Ads

Header ADS

Ofisa TRC aliyepinga tozo za miamala ya simu afukuzwa kazi



Wakati kilio cha tozo za miamala kikiendelea mtaani, Shirika la Reli Tanzania (TRC) limemfukuza kazi meneja wake wa kanda ya Dar es Salaam, Jonas Afumwisye kwa kuzipinga kwenye makundi ya kijamii.
Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Masanja Kadogosa alimwandikia barua Afumwisye kumjulisha kuhusu uamuzi huo Agosti 19 baada ya kuthibitika kwa tuhuma zilizokuwa zikimkabili.
Afumwisye amekiri kupokea barua hiyo juzi Agosti 22, ila akasema anakusudia kukata rufaa Tume ya Utumishi wa Umma kama sheria inavyoelekeza.
“Ni kweli nimepata hayo matatizo…utaratibu unaofuata ni kukata rufaa ndani ya siku 45, ” alisema Afumwisye alipoulizwa.
Barua hiyo inaeleza kuthibitishwa kwa tuhuma za Afumwisye kwenda kinyume na kanuni ya 42 jedwali la kwanza, sehemu A kipengele cha 10 cha kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2003.
“Kati ya Julai 10 na Septemba 25 mwaka 2021, kupitia makundi ya kijamii, ulipinga juhudi za Serikali kuanzisha tozo kwenye miamala ya simu,” inasomeka barua ya Kadogosa.
Ofisa huyo pia anatuhumiwa kupinga juhudi za Serikali kuwapa chanjo wananchi kuepuka milipuko ya magonjwa. Kosa jingine Kadogosa amesema ni kukashfu viongozi wakuu wa nchi akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan na Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson kupitia makundi ya kijamii.
“Kutokana na tuhuma zote kuthibitika, bodi ya wakurugenzi wa shirika kwa mamlaka iliyopewa chini ya kifungu cha 13(f) cha Sheria ya Reli namba 10 ya mwaka 2017 imeamua ufukuzwe kazi kuanzia Agosti 19, 2022. Endapo hautaridhika na uamuzi huu, unayo haki ya kukata rufaa Tume ya Utumishi wa Umma ndani ya siku 45 kuanzia tarehe ya kupokea barua hii. Hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 60 ya kanuni za utumishi wa umma za mwaka 2003,” inaeleza barua hiyo iliyosainiwa na Kadogosa

No comments

Powered by Blogger.