Header Ads

Header ADS

Polisi Wanawake Mkoa wa Manyara wamchangia sh,500,000/= Emanuel john kwaajili ya kwenda Hospitalini



Mkazi wa Mjini Babati, Emmanuel John anayesumbuliwa na tatizo la kupumua baada ya kuota nyama puani, amechangiwa sh500,000/= na polisi wanawake wa Mkoa wa Manyara, kwa ajili ya kupelekwa hospitalini.

Mkuu wa kikosi cha usalama barabarani Mkoa wa Manyara, (RTO) Mrakibu mwandamizi wa polisi (SSP) Georgina Richard Matagi akizungumza wakati akikabidhi fedha hizo amesema askari wanawake hao wamechanga fedha hizo kwa hiyari yao.

RTO Matagi amesema yeye akiwa kiongozi wa askari wanawake wa mkoa huo aliwaeleza tatizo hilo wenzake na wakachanga ili kumsaidia raia huyo anayeishi mjini Babati.

Amesema askari wa kike walijitolea kumchangia mgonjwa huyo sh200,000 na kumkatia bima ya afya na matumizi mengine.

Amesema kutokana na bima ya afya itaanza kutumika baada ya mwezi mmoja askari hao wa kike wakawa na moyo wa upendo wakaongeza mchango wa fedha nyingine sh310,000 ambazo zitamsaidia akipatiwa matibabu.

"Tumemuombea kibali askari wa kike inspekta kimario kwa kamanda wa polisi wa mkoa wa Manyara, afande RPC George Katabazi ili amsindikize mgonjwa akiwa Arusha na kumsaidia kwa siku mbili tatu ili awe naye kisha atarudi," amesema RTO Matagi.

Amesema wao kama polisi wa wanawake wa mkoa huo waliamua kumchangia kiasi hicho cha fedha kwa hiyari yao wenyewe baada ya kupata taarifa ya ugonjwa wake.

“Tunatarajia mara baada ya kupatiwa matibabu atapona na kuwa na afya njema ili aweze kuendelea na maisha yake ya kila siku hapa mjini Babati,” amesema RTO Matagi.

Kwa upande wake mgonjwa huyo Emmanuela John amewashukuru askari hao wanawake kwa kumchangia kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kupata matibabu.

"Nawashukuru wote kwa ujumla kwa kujitolea kwao ili niweze kwenda kupatiwa matibabu kwenye hospitali ya rufaa ya Mount Meru jijini Arusha," amesema Emmanuela.

No comments

Powered by Blogger.