Header Ads

Header ADS

Urusi yatuma majeshi yake Ukraine na kuyatambua maeneo yaliojitenga kama mataifa huru

 Rais wa Urusi Vladimir Putin ametambua maeneo ya waasi yaliyojitenga mashariki mwa Ukraine kama mataifa huru, na hivyo kumaliza mazungumzo ya amani huko.
Jamuhuri za watu zilizojitangaza za Donetsk na Luhansk ni nyumbani kwa waasi wanaoungwa mkono na Urusi ambao wamekuwa wakipigana na vikosi vya Ukraine tangu 2014.
Wanajeshi wa Urusi wameagizwa kufanya kile kinachoitwa "kazi za kulinda amani" katika mikoa yote miwili.
Rais wa Ukraine aliishutumu Urusi kwa kukiuka mamlaka yake kimakusudi.
Katika hotuba yake ya televisheni usiku wa manane kwa taifa, Rais Volodymyr Zelensky alisema Ukraine inataka amani, lakini akatangaza kwamba "Hatuogopi" na "haitatoa chochote kwa mtu yeyote". Kyiv sasa inahitaji "hatua wazi na madhubuti ya msaada" kutoka kwa washirika wake wa kimataifa.
"Ni muhimu sana kuona sasa rafiki na mshirika wetu wa kweli ni nani, na ni nani ataendelea kutisha Shirikisho la Urusi kwa maneno tu," aliongeza.
Mataifa yenye nguvu ya Magharibi yanahofia kutambua kwa Bw Putin kwa maeneo yanayodhibitiwa na waasi kunafungua njia kwa wanajeshi wa Urusi kuingia rasmi mashariki mwa Ukraine.
Katika miaka ya hivi karibuni, pasi za kusafiria za Urusi zimetolewa kwa idadi kubwa ya watu huko Donetsk na Luhansk, na washirika wa Magharibi wanahofia kuwa Urusi sasa inaweza kuhamisha vitengo vya kijeshi kwa kisingizio cha kuwalinda raia wake.
Akizungumza katika hotuba ya saa moja mara baada ya tangazo la Jumatatu, Bw Putin alisema Ukraine ya kisasa "iliundwa" na Urusi ya Usovieti, akiitaja nchi hiyo "ardhi ya Urusi ya kale".
Alitaja Urusi kuwa "imeibiwa" wakati wa kuanguka kwa Umoja wa Kisovieti mwaka 1991, akiishutumu Ukraine kuwa "koloni la Marekani" linaloendeshwa na serikali ya vibaraka, na alidai kuwa watu walikuwa wakiteseka chini ya uongozi wake wa sasa. Alitaja maandamano ya 2014 ambayo yalimwondoa kiongozi wa Ukraine anayeunga mkono Urusi kama mapinduzi.


No comments

Powered by Blogger.