Header Ads

Header ADS

Kesi yanguruma Mwaikali akipinga kusimikwa askofu mpya wa Konde


Hatimaye kesi ya Dk Edward Mwaikali askofu aliyeondolewa katika Dayosisi ya Konde ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kupinga kusimikwa kwa askofu mpya, Geofrey Mwakihaba imeanza kuunguruma.

kesi pic


Kesi hiyo ilianza kusikilizwa juzi katika Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya, mbele ya Jaji James Karayemaha ambapo wawasilisha maombi walieleza sababu ya kupinga kusimikwa kwa Mwakihaba.

Wakili anayeuwakilisha upande wa Mwaikali, Godwin Mussa alieleza sababu za pingamizi hilo kuwa ni kulinda haki ya mtu mmojammoja ili kuepuka vurugu zinazoweza kujitokeza wakati wa kusimikwa kwa askofu mteule hapo Juni 5.

“Mheshiniwa jaji endapo hakutakuwapo zuio lolote, Kanisa la KKKT litakuwa likiongozwa na maaskofu wawili kwa kuwa kuondolewa kwa Askofu Mwaikali hakukufuata taratibu na kanuni za katiba ya kanisa,” alisema.

Wakili Mussa aliongeza kuwa migogoro iliyopo kwenye jamii ni mikubwa hivyo ni vyema mahakama ikarejea maombi yaliyowasilishwa ikiwa ni pamoja na kupinga kulazimishwa kurejesha vifaa vya Askofu Dk Mwaikali.

Aidha aliiomba mahakama kuangalia pingamizi la kisheria kwamba mleta maombi, Askofu Mwaikali alituhumiwa bila kupewa nafasi ya kusikilizwa na kutolewa katika nafasi yake bila kufuata taratibu, kanuni na katiba ya Dayosisi ya Konde.

 

Wakili Mussa aliongeza kuwa mahakama ina haki ya kusikiliza maombi yaliyowasilishwa kwa kuwa ni chombo chenye kutoa haki na si kuingilia migogoro ya kidini.

Akijibu maombi hayo, wakili wa wajibu maombi, Dk Daniel Palangyo aliiomba mahakama kulitupilia mbali ombi hilo kwa kuwa Askofu Mwaikali hakufuata taratibu za kanisa kufungua kesi mahakamani hapo.

Aidha alimtaka mleta maombi awasilishe vielelezo mahakamani kwa nini hakulalamika kwenye Mkutano Mkuu wa Kanisa chini ya kifungu cha Sheria 13 cha mwaka 2015.

Alisema hawapingani na hoja ya Mwaikali bali wanamshauri afuate utaratibu uliowekwa chini ya katiba ya kanisa kabla ya kulipeleka shauri hilo mahakamani.

“Mahakama ione hoja ya msingi ya kuyatupilia mbali maombi hayo na mleta maombi atatakiwa kulipa gharama,” alisema.

Baada ya kusikiliza maelezo ya panda zote, Jaji Karayemaha aliwataka viongozi hao wa dini kutotengeneza chuki na maneno yanayowasilishwa mahakamani yazingatie vifungu vya Biblia.

Alisema wanapaswa kukaa meza moja kulinda amani na kufanya maamuzi mazuri na kuachana na chuki, maneno makali kwa kuwa wao ni wamoja na ipo siku watadumu pamoja.

Jaji Karayemaha alisema ufike wakati washirikiane na vyombo vya dola hususani Jeshi la Polisi kuitafuta amani, kutathimini utu na kufurahia maisha.

Jaji huyo alihairisha kesi hiyo mpaka kesho itakapotajwa tena na kuanza kupitia maombi ya pingamizi lililotolewa.

 

No comments

Powered by Blogger.